Leviticus 7

Sadaka Ya Hatia

1 a“ ‘Haya ndiyo masharti kwa ajili ya sadaka ya hatia, ambayo ni takatifu sana: 2Sadaka ya hatia itachinjiwa mahali pale ambapo sadaka ya kuteketezwa huchinjiwa, nayo damu yake itanyunyizwa pande zote za madhabahu. 3 bMafuta yake yote yatatolewa sadaka: mafuta ya mkia na mafuta yale yanayofunika sehemu za ndani, 4 cfigo zote mbili pamoja na mafuta yanayozizunguka yaliyo karibu na kiuno na yale yanayofunika ini, ambayo yataondolewa pamoja na hizo figo. 5 dKuhani atayateketeza juu ya madhabahu kuwa sadaka iliyotolewa kwa Bwana kwa moto. Hii ni sadaka ya hatia. 6 eMwanaume yeyote katika jamaa ya kuhani aweza kuila, lakini lazima iliwe mahali patakatifu; ni takatifu sana.

7 f“ ‘Sheria hii ya sadaka ya hatia ni sawasawa na ile ya sadaka ya dhambi: Nyama ya yule mnyama aliyetolewa sadaka ni ya yule kuhani anayesimamia ibada ya upatanisho. 8Kuhani anayetoa sadaka ya kuteketezwa kwa ajili ya mtu yeyote anaweza kuichukua ngozi ya mnyama yule aliyetolewa iwe yake. 9 gKila sadaka ya nafaka iliyookwa jikoni au kupikwa katika sufuria au katika kikaangio itakuwa ya kuhani anayeitoa. 10Nayo kila sadaka ya nafaka, iwe imechanganywa na mafuta au iko kavu, itakuwa ya wana wa Haruni, nayo itagawanywa sawa kati yao.

Sadaka Ya Amani

11“ ‘Haya ndiyo masharti kwa ajili ya sadaka ya amani ambayo mtu aweza kuileta kwa Bwana:

12 h“ ‘Ikiwa mtu atatoa sadaka ya amani kwa ajili ya kuonyesha shukrani, pamoja na sadaka hii ya shukrani, atatoa maandazi yasiyotiwa chachu yaliyochanganywa na mafuta, mikate myembamba isiyotiwa chachu iliyopakwa mafuta, maandazi ya unga laini uliokandwa vizuri na kuchanganywa na mafuta. 13 iPamoja na sadaka hii ya amani ya shukrani ataleta sadaka ya maandazi yaliyotengenezwa kwa chachu. 14 jAtaleta moja ya kila aina ya andazi kama sadaka, matoleo kwa Bwana; hii ni ya kuhani anayenyunyiza damu ya sadaka ya amani. 15 kNyama ya sadaka ya amani kwa ajili ya shukrani lazima iliwe siku iyo hiyo inapotolewa; hutabakiza kitu chochote mpaka asubuhi.

16 l“ ‘Lakini kama sadaka yake ni kwa ajili ya nadhiri au ni sadaka ya hiari, sadaka hiyo italiwa siku hiyo inapotolewa, lakini chochote kinachobakia kinaweza kuliwa kesho yake. 17 mNyama yoyote ya sadaka inayobaki mpaka siku ya tatu lazima iteketezwe kwa moto. 18 nKama nyama yoyote ya sadaka ya amani italiwa siku ya tatu, Bwana hataikubali. Haitahesabiwa kwake huyo aliyeitoa, kwa kuwa ni najisi. Mtu atakayekula sehemu yake yoyote atahesabiwa hatia.

19“ ‘Nyama ile inayogusa chochote ambacho ni najisi kwa kawaida ya ibada kamwe haitaliwa, ni lazima iteketezwe kwa moto. Kuhusu nyama nyingine, mtu yeyote aliye safi kwa kawaida ya ibada anaweza kuila. 20 oLakini kama mtu yeyote najisi akila nyama yoyote ya sadaka ya amani iliyotolewa kwa Bwana, huyo mtu lazima akatiliwe mbali na watu wake. 21 pKama mtu yeyote akigusa kitu kilicho najisi, iwe ni uchafu wa mwanadamu, au mnyama najisi, au kitu chochote kilicho najisi, kitu cha kuchukiza, kisha akala nyama yoyote ya sadaka ya amani iliyotolewa kwa Bwana, mtu huyo ni lazima akatiliwe mbali na watu wake.’ ”

Kula Mafuta Na Kunywa Damu Kwakatazwa

22Bwana akamwambia Musa, 23 q“Waambie Waisraeli: ‘Msile mafuta yoyote ya ng’ombe, kondoo wala mbuzi. 24 rMafuta ya mnyama aliyekutwa amekufa au ameraruliwa na mnyama pori yanaweza kutumika kwa kazi nyingine yoyote, lakini kamwe msiyale. 25Mtu yeyote alaye mafuta ya mnyama ambaye ametolewa sadaka kwa Bwana kwa moto ni lazima akatiliwe mbali na watu wake. 26 sPopote mtakapoishi, kamwe msinywe damu ya ndege yeyote wala ya mnyama. 27 tIkiwa mtu yeyote atakunywa damu, mtu huyo lazima akatiliwe mbali na watu wake.’ ”

Fungu La Makuhani

28Bwana akamwambia Musa, 29“Waambie Waisraeli: ‘Mtu yeyote aletaye sadaka ya amani kwa Bwana ataleta sehemu ya sadaka hiyo kama dhabihu yake kwa Bwana. 30 uAtaleta sadaka kwa mikono yake mwenyewe iliyotolewa kwa Bwana kwa moto; ataleta mafuta ya huyo mnyama pamoja na kidari, naye atainua hicho kidari mbele za Bwana kuwa sadaka ya kuinuliwa. 31 vKuhani atayateketeza hayo mafuta juu ya madhabahu, lakini kidari kitakuwa cha Haruni na wanawe. 32 wPaja la kulia la sadaka zako za amani utampa kuhani kama matoleo. 33Mwana wa Haruni atoaye damu na mafuta ya sadaka ya amani ndiye atakayepewa paja hilo la kulia kuwa fungu lake. 34 xKutoka kwenye sadaka za amani za Waisraeli, mimi Mungu nimepokea kidari kile kilichoinuliwa pamoja na lile paja lililotolewa, nami nimevitoa kwa kuhani Haruni na wanawe kuwa fungu lao la kawaida kutoka kwa Waisraeli.’ ”

35Hii ndiyo sehemu ya sadaka zilizotolewa kwa Bwana kwa moto, ambazo zilitengwa kwa ajili ya Haruni na wanawe siku ile walipowekwa wakfu ili kumtumikia Bwana katika kazi ya ukuhani. 36 ySiku ile walipotiwa mafuta, Bwana aliagiza kwamba Waisraeli wawape hili kama fungu lao la kawaida kwa vizazi vijavyo.

37 zBasi haya ndiyo masharti kuhusu sadaka ya kuteketezwa, sadaka ya nafaka, sadaka ya dhambi, sadaka ya hatia, sadaka ya kuwekwa wakfu, na sadaka ya amani, 38 aaambayo Bwana alimpa Musa juu ya Mlima Sinai siku ile alipowaagiza Waisraeli walete sadaka zao kwa Bwana, katika Jangwa la Sinai.
Copyright information for SwhKC